17/04/2018
MFUKO WA RIWAYA WA UWARIDI (UWARIDI RIWAYA FUND)
Mnamo tarehe 23 Februari mwaka huu wa 2018 tuliweka andiko kwenye huu ukurasa wetu lililosomeka “TUNA NDOTO”. Andiko lile lilibainisha ndoto yetu ya kuona watunzi wengi wakiweza kuchapa vitabu na kuweka majina yao kwenye ramani ya fasihi andishi nchini na duniani kupitia riwaya; na pia kuona waandishi wenye ndoto za siku moja kuweza kuchapa vitabu vyao wao wenyewe, wanatimiza ndoto zao.
Sasa ndoto hii IMETIMIA.
Naam, imetimia, kwani sasa UWARIDI imeanza kuiishi ndoto hii kwa kuanzisha mfuko maalum wa kufadhili uchapaji wa riwaya bora kwa ajili ya wanachama wake walioridhia kujiunga na mfuko huo, kupitia MFUKO WA RIWAYA WA UWARIDI.
Hii inamaanisha kuwa juhudi za kuanzisha MFUKO huu zilikuwa zimeshaanza tangu wakati wa andiko lile, na sasa tunadhani ni wakati muafaka kuubainisha rasmi kwenu.
Kwa kutambua kuwa uwezo wa wanachama wetu kuweza kuchapa vitabu ni mdogo na kuwa mazingira sio mepesi kuwawezesha wengi miongoni mwao kumudu gharama za kuchapa vitabu vyao wao mwenyewe, UWARIDI imebuni utaratibu huu wa MFUKO WA RIWAYA WA UWARIDI kwa lengo la wanachama wake kuwezeshana wao kwa wao, kuchapa vitabu.
MFUKO huu umebuniwa ni kwa mujibu wa ibara ya 17 (ix) ya Katiba ya UWARIDI, ambayo inataja moja ya kazi za Umoja kuwa ni:
“Kusimamia ufadhili, kuchangisha fedha na kusaka misaada ya kuwezesha shughuli za umoja na waandishi.”
DHUMUNI KUU la MFUKO huu ni kuwezesha wanachama wa UWARIDI kuchapa vitabu bora na kuweka majina yao kwenye ramani ya fasihi andishi nchini na duniani kupitia riwaya.
LENGO KUU la MFUKO huu ni kuweka mfumo wa waandishi wa riwaya (wanachama wa UWARIDI) kuwezeshana wao kwa wao, kuchapa nakala nyingi za vitabu, kwa gharama nafuu na kwa kufuata ratiba maalumu.
Kupitia MFUKO huu, wanachama washiriki watafadhiliwa gharama zifuatazo, kwa hela walizochangishana wao wenyewe:
1. Uhariri
2. Usanifu wa Kurasa (Layout)
3. Usanifu wa Jalada
4. Uchapaji
5. Matangazo (Facebook, Instagram, Magazeti)
Kufikia sasa wanachama walioamua kushirki kwenye MFUKO huu wameshachangishana fedha za kumuwezesha mmoja wetu kuchapa kitabu chake na kukiingiza sokoni. UWARIDI itasimamai mauzo na usambazaji wa vitabu vyote vitakavyolewa chini ya MFUKO huu, kila kona ya nchi hii.
Mauzo ya kitabu husika yakifikisha kiwango cha fedha iliyotolewa kufadhili kitabu cha kwanza, atapewa mwandishi wa pili kwenye utaratibu ili naye atoe kitabu chake… na mzunguko utaendelea kwa namna hiyo.
Ndani ya utaratibu huu, tunatarajia kutoa kitabu kipya kutoka kwa mwandishi mpya kila mwezi.
Katika siku chache zijazo tutawatangazia waandishi watakaoanza kunufaika na MFUKO huu, kwa awamu ya kwanza ya utekelezaji wake, na kazi zao.
TUNAWAOMBA, mziunge mkono hatua hizi za kueneza fasihi andishi nchini kwa kununua kwa wingi nakala za vitabu tutakavyovitangaza chini ya MFUKO huu, ili nanyi muwe chachu ya maendeleo ya fasihi andishi nchini na kuwatia moyo waandishi wetu.
Ni imani ya UWARIDI kuwa Mfuko huu utakuwa daraja muhimu la kuwafikisha wanachama wake wenye dira, kwenye timizo halisi la ndoto zao za kiuandishi.
UWARIDI…NJOO TUNUKIE!